Kuharibika mimba

Imepitiwa/Imerekebishwa May 2023

Je, kuharibika mimba ni nini?

Kuharibika kwa mimba ni wakati ujauzito wako unaisha kabla ya wiki 20 za ujauzito. Mimba nyingi huharibika katika wiki 12 za kwanza za ujauzito.

  • Kutokwa na damu na tumbo kusokota ni dalili za kawaida za mimba kuharibika

  • Ikiwa ulikuwa mjamzito na bado haukuwa unajua, mimba yako inaweza kuharibika na ukafikiria tu kuwa ni hedhi yako

  • Ili kujua kama mimba yako imeharibika, madaktari wataangalia mlango wako wa kizazi (sehemu ya chini ya uterasi yako)

  • Madaktari watakufanyia pia kipimo cha picha kutumia mawimbi ya sauti (picha za sehemu tofauti za ndani ya uterasi yako, pia huitwa tumbo lako la uzazi)

  • Wanawake wengi ambao wamebaribikiwa na mimba moja hupata ujauzito tena na kujifungua watoto wenye afya nzuri

  • Hata hivyo, uwezekano wa mimba yako kuharibika huongezeka kila mara: kadiri mimba zako zinavyoharibika, ndivyo uwezekano wako wa kuharibikiwa mimba tena huongezeka

  • Ikiwa mimba zako zimeharibika mara kadhaa, itakuwa vyema kwako kumuona daktari kabla ya kubeba tena ujauzito

  • Madaktari wanaweza kujaribu kufanya mimba yako ifuatayo kufanikiwa

Je, mimba kuharibika husababishwa na nini?

Madaktari huwa hawajui kinachosababisha mimba kuharibika. Mimba kuharibika hakusababishwi na mshtuko wa ghafla wa kihisia, kama vile kupata habari mbaya. Pia, majeraha madogo kama vile kuteleza na kuanguka hayasababishi mimba kuharibika. Hata hivyo, majeraha makubwa kama vile ajali mbaya ya gari yanaweza husababisha mimba kuharibika.

Sababu za mimba kuharibika katika wiki 12 za kwanza za ujauzito

  • Tatizo la kijusi, kama vile kasoro ya kuzaliwa au ugonjwa wa kurithi

Wakati mwingine kijusi kina kasoro ambayo ni sugu sana hadi kuwa kijusi hakiwezi kuishi zaidi ya mwezi mmoja au miwili ndani yako. Kasoro kubwa sana husababisha mimba nyingi kuharibika katika wiki 12 za mwanzo wa ujauzito.

Sababu za mimba kuharibika katika wiki 13 hadi 20 za ujauzito

Mara nyingi, madaktari hawagundui sababu ya kuharibika kwa mimba katika hatua hii. Lakini wakati mwingine wanaweza kubainisha mojawapo ya haya kama chanzo:

Sababu za mimba kuharibika mara kwa mara

Ikiwa umeharibikiwa na mimba mara kadhaa, madaktari watatafuta matatizo kama vile:

  • Damu inayoganda kwa urahisi sana kwa mwanamke

  • Kromosomu isiyo ya kawaida katika kijusi kutoka kwa mzazi yeyote

Je, dalili za mimba kuharibika ni zipi?

Mimba kuharibika mapema katika ujauzito kunaweza kuonekana kama hedhi ya kawaida. Ikiwa hukujua kuwa ulikuwa mjamzito, kuna uwezekano mkubwa kuwa hutajua kuwa mimba yako imeharibika.

Wakati mwingine dalili hujitokeza wazi:

  • Damu nyekundu angavu au iliyokolea

  • Tumbo kusokota

  • Kupitisha madonge makubwa ya damu iliyoganda na vipande vya tishu

Mara ya kwanza unaweza kuwa unatokwa na damu kidogo tu, iliyo sawa na kupata hedhi yako. Mimba inapoendelea kuharibika, kwa kawaida hali ya kutokwa na damu huzidi kuwa mbaya. Damu inaweza kuwa nyekundu angavu au iliyokolea. Wakati mwingine unaweza pia kutokwa na madonge ya damu. Utakuwa na hali ya kukakamaa kwa tumbo ambayo inaweza kuwa mbaya zaidi wakati uterasi (tumbo la uzazi) yako inasukuma nje vipande na vipande vidogo vya ujauzito.

Mpigie simu daktari wako mara moja ikiwa unavuja damu wakati wa ujauzito wako. Si wakati wote kutokwa na damu wakati wa ujauzito kunamaanisha kuwa mimba inaharibika. Takriban nusu ya visa hivyo, ujauzito unaendelea vizuri. Hata hivyo, daktari wako anahitaji kuchunguza ili kuona ikiwa ujauzito uliharibika au la. Ikiwa unapitisha mabonge makubwa au vipande vidogo vya tishu, viweke kwenye chombo au vifunge kwa taulo ili daktari achunguze.

Je, madaktari wanawezaje kujua ikiwa mimba yangu imeharibika?

Ikiwa umetokwa na damu au tumbo kusokota katika kipindi cha wiki 20 za kwanza za ujauzito wako, madaktari:

  • Watafanya uchunguzi wa fupanyonga: Wataangalia ndani ya uke wako (njia ya uzazi) ili kuangalia mlango wako wa kizazi (sehemu ya chini ya uterasi ambapo mtoto wako anatokea)—ikiwa mlango wako wa kizazi uko wazi, kuna uwezekano wa mimba kwa kuharibika.

  • Fanya kipimo cha picha kutumia mawimbi ya sauti: Kipimo hiki kinatumia mawimbi ya sauti kutengeneza picha za sehemu tofauti za ndani ya uterasi yako—kinaweza kuonyesha ikiwa kijusi kingali hai

  • Fanya vipimo vya damu: Madaktari huchunguza viwango vyako vya homoni ya ujauzito ya hCG

Je, madaktari hutibu vipi kuharibika mimba?

Ikiwa kijusi na kondo la nyuma (kiungo kinacholisha kijusi) havipo tena katika mwili wako, hutahitaji matibabu yoyote. Kutokwa na damu na kukakamaa kutaisha baada ya muda mfupi.

Ikiwa vipande vidogo na vipande vya ujauzito bado viko kwenye mwili wako, madaktari wanaweza:

  • Kuchunguza ili kuona ikiwa uterasi yako itatoa chembechembe zilizobaki yenyewe, ilimradi tu huna homa au hauonekani kuwa mgonjwa

  • Watafanya utaratibu wa kuondoa ujauzito uliobaki

Ikiwa madaktari watahitaji kuondoa vipande vya ujauzito wako kutoka kwa uterasi yako, watakupa dawa ya kukufanya upate usingizi. Utaratibu utakaofanywa unategemea ujauzito uko katika hatua gani:

  • Katika wiki 12 za kwanza za ujauzito: Kuondoa vipande kwa kutumia chombo cha kunyonya kinachowekwa kwenye uterasi yako kupitia uke wako

  • Kati ya wiki 12 na 20 za ujauzito: Kuondoa vipande kwa kutumia vyombo vya upasuaji vinavyowekwa kwenye uterasi yako kupitia uke wako

  • Ikiwa ni karibu na wiki 20 za ujauzito: Unaweza kupewa dawa ya kuanzisha uchungu wa uzazi ili kupitisha ujauzito uliobaki

Je, ninawezaje kuzuia mimba kuharibika?

Kwa kweli huwezi kuzuia mimba kuharibika Ikiwa umekuwa ukitokwa na damu au tumbo kusokota katika kipindi cha wiki 20 za kwanza za ujauzito wako, daktari wako anaweza kukuambia uepuke shughuli nyingi za kimwili na upumzike. Lakini hakuna uthibitisho kuwa vitu hivi vinasaidia.

Ninawezaje kuhisi vyema baada ya mimba kuharibika?

Ni jambo la kawaida kuhisi huzuni, hasira, na hatia baada ya kuharibika kwa mimba.

  • Zungumza na mtu mwingine ukiwa na huzuni na masikitiko kwa kupoteza ujauzito wako

  • Ikiwa una wasiwasi kuhusu kuharibika kwa mimba nyingine, zungumza na daktari ambaye anaweza kujadili vipimo vinavyoweza kufanywa

  • Kumbuka kuwa wanawake wengi wanaoharibikiwa na mimba hupata ujauzito tena na kuzaa watoto wenye afya nzuri