Ujauzito wa Nje ya Kizazi

Imepitiwa/Imerekebishwa May 2023

Je, ujauzito wa nje ya kizazi ni nini?

  • Ujauzito wa nje ya kizazi ni wakati yai lililorutubishwa linapojishikilia mahali pasipofaa, kama vile kwenye mirija ya uzazi

  • Ujauzito wa nje ya kizazi hausababishi mtoto kuzaliwa

  • Ikiwa haijatambuliwa na kutibiwa mara moja, inaweza kusababisha kutokwa na damu inayotishia maisha ya mwanamke

Katika ujauzito wenye afya, mbegu ya kiume huingia (inarutubisha) yai huku yai likiwa kwenye moja ya mirija yako ya uzazi. Mirija yako ya uzazi inaunganisha ovari zako (mahali mayai yako yanapohifadhiwa) na uterasi yako (tumbo la uzazi). Yai lililorutubishwa, ambalo liko kwenye kifuko, kisha huhamia kwenye uterasi yako na kujishikilia hapo ili likue.

Ectopic Pregnancy: A Mislocated Pregnancy

Normally, an egg is fertilized in the fallopian tube and becomes implanted in the uterus. However, if the tube is narrowed or blocked, the egg may move slowly or become stuck in the fallopian tube. The fertilized egg may never reach the uterus, resulting in an ectopic (mislocated) pregnancy.

An ectopic pregnancy may be located in many different places, including a fallopian tube, an ovary, the cervix, and the abdomen.

Katika ujauzito wa nje ya kizazi yai lililorutubishwa halijipandikizi kwenye uterasi yako. Badala yake, linajipandikiza mahali pengine. Inaweza kujipandikiza kwenye mojawapo ya mirija yako ya uzazi, kwenye ukuta wa uterasi yako, au kwenye tumbo lako nje ya uterasi yako.

  • Yai lililorutubishwa haliwezi kukua ipasavyo nje ya uterasi yako

  • Kifuko kinachoshikilia yai kitapasuka, kwa kawaida baada ya wiki 6 hadi 16 kutoka wakati wa kupata ujauzito

  • Kifuko kinapopasuka, unatokwa na damu nyingi

  • Kijusi hakiishi

  • Ujauzito wa nje ya kizazi unaweza kusababisha maumivu ya sehemu ya chini ya tumbo na kutokwa damu ukeni

  • Ikiwa haitatibiwa, ujauzito wa nje ya kizazi huhatarisha maisha

  • Wakati mwingine dalili huanza kabla hata hujajua kuwa wewe ni mjamzito

  • Ili kuokoa maisha yako, madaktari hufanya upasuaji au kukupa dawa ya kupunguza ukubwa wa ujauzito wa nje ya kizazi

Je, dalili za ujauzito wa nje ya kizazi ni zipi?

Ikiwa kifuko chenye yai hakijapasuka, huenda usiwe na dalili, au unaweza kuwa nayo:

  • Kutokwa na damu au kuwa na madoadoa ya damu yanayotoka kwenye uke wako

  • Kusokota au maumivu kwenye sehemu ya chini ya tumbo

Ikiwa kifuko kilichoshikilia yai kitapasuka, unaweza kuwa na:

  • Maumivu makali, yanayoendelea kwenye sehemu ya chini ya tumbo

  • Kutokwa na damu nyingi kwenye uke wako (njia ya uzazi)

  • Kutokwa na damu nyingi ndani ya tumbo lako (mahali ambapo hapaonekani)

Kutokwa na damu nyingi kunaweza kusababisha kuzirai, kutokwa na jasho, au hisia ya kizunguzungu. Shinikizo lako la damu linaweza kupungua sana (hali inayoitwa mshtuko), na unaweza kuaga dunia.

Je, madaktari wanawezaje kujua ikiwa nina ujauzito wa nje ya kizazi?

Ikiwa una umri wa kuzaa na una maumivu katika sehemu ya chini ya tumbo au kutokwa na damu ukeni, kuzimia, au kupata mshtuko, daktari wako atakufanyia kipimo cha ujauzito. Ikiwa kipimo cha ujauzito kina matokea chanya au unajua kuwa wewe ni mjamzito:

Kipimo cha picha kinachotumia mawimbi ya sauti hutumia mawimbi ya sauti kutengeneza picha zinazosonga za sehemu za ndani za mwili wako. Kwa kawaida daktari anaweza kuona ikiwa ujauzito uko kwenye uterasi yako au la. Hata hivyo, ikiwa ni mapema katika ujauzito wako, daktari anaweza kukosa kupata kijusi kwa kutumia kipimo cha picha kinachotumia mawimbi ya sauti. Kisha daktari wako ataamua cha kufanya kulingana na dalili zako na ni kiasi cha homoni ya ujauzito kilichopo katika damu yako.

Ikiwa dalili zako ni kali, daktari anaweza kukata sehemu kidogo chini ya kitovu chako na kuingiza bomba la kuona (laparoskopi) ili kutafuta ujauzito wa nje ya kizazi.

Je, madaktari hutibu vipi ujauzito wa nje ya kizazi?

Ujauzito wa nje ya kizazi sharti usitishwe haraka iwezekanavyo ili kuokoa maisha ya mwanamke.

Dawa

Ikiwa ujauzito wa nje ya kizazi haujapasuka na bado ni mdogo, madaktari wanaweza kukudunga sindano ya dawa iitwayo methotrexate. Dawa hii husababisha ujauzito wa nje ya kizazi kupungua na kutoweka. Wakati mwingine methotrexate haifanyi kazi na utahitaji upasuaji.

Upasuaji

Kwa kawaida, watafanya upasuaji ili kuondoa ujauzito wa nje ya kizazi. Mara nyingi wao hufanya upasuaji kwa kutumia bomba nyembamba (laparoskopi). Ikiwezekana, daktari wako atatoa ujauzito wa nje ya kizazi pekee.

Ikiwa ujauzito wa nje ya kizazi uko kwenye mrija wako wa uzazi, wakati mwingine daktari anaweza kulazimika kuondoa mrija wa uzazi pia.