Ketoasidosisi ya Kisukari

Imepitiwa/Imerekebishwa Mar 2023

Kisukari ni ugonjwa ambao viwango vyako vya sukari kwenye damu (glukosi) kuwa juu sana.

Je, ketoasidosisi ya kisukari (DKA) ni nini?

Ketoasidosisi ya kisukari ni tatizo kubwa la kisukari. Mara nyingi huitwa DKA.

Ukiwa na DKA, kiwango cha sukari kwenye damu yako hupanda, asidi inayoitwa ketoni hujaa katika damu yako, unapoteza majimaji mengi, na utendakazi wa mwili wako haufanyi kazi vizuri. Unahitaji matibabu mara moja.

  • Watu wenye kisukari cha aina ya 1 wana uwezekano mkubwa wa kuwa na DKA

  • DKA inaweza kuwa dalili ya kwanza kuwa una kisukari

  • Matibabu hujumuisha majimaji na insulini inayodungiwa kwenye mshipa wa damu

  • Bila matibabu, DKA inaweza kusababisha kupoteza fahamu na kifo

Je, DKA husababishwa na nini?

Mwili wako unahitaji insulini ili kutumia sukari iliyo kwenye damu kwa ajili ya kupata nguvu. Ikiwa huna insulini ya kutosha (kwa mfano, kwa sababu una kisukari cha aina ya 1 ambacho hakijatibiwa), kiwango cha sukari kwenye damu yako hupanda sana kwa sababu sukari haiwezi kuingia kwenye seli zako. Badala yake mwili wako huchoma mafuta kwa ajili ya kupata nguvu za mwili. Mafuta yaliyochomwa huenda kwenye ini yako na kugeuzwa kuwa asidi inayoitwa ketoni. Ketoni hujaa kwenye damu na mkojo wako.

Kiwango cha juu cha ketoni katika damu yako kinaweza kukufanya kuwa mgonjwa sana.

Ikiwa una kisukari, kuna uwezekano mkubwa wa wewe kupata DKA ikiwa:

  • Utaacha kutumia insuliniyako

  • Utaacha kufuata lishe yako kwa kuwa insulini unayotumia haitoshi

  • Utakuwa mgonjwa, na mwili wako uko chini ya mkazo

Vichocheo vya kawaida vya DKA ni pamoja na:

Je, dalili za DKA ni zipi?

Dalili zinajumuisha:

  • Kiu isiyo ya kawaida

  • Kukojoa sana kuliko kawaida

  • Kupoteza uzani bila sababu dhahiri

  • Kuhisi mgonjwa kwenye tumbo lako au kutapika

  • Kuhisi udhaifu na uchovu

  • Maumivu ya tumbo

  • Kuvuta pumzi nzito, kwa haraka

  • Harufu ya mdomo iliyo na harufu kama ya matunda (kama vile kiondoa rangi za kucha)

DKA inaweza kupelekea kupoteza fahamu au kifo ikiwa haitatibiwa.

Je, madaktari wanawezaje kujua ikiwa nina DKA?

Madaktari hufanya:

  • Vipimo vya damu ili kuchunguza sukari kwenye damu yako, viwango vya ketoni katika damu yako, na viwango vya baadhi ya elektroliti (madini, kama vile sodiamu na potasiamu, ambayo husaidia katika utendaji kazi mwingi muhimu mwilini)

Ili kupata matatizo ambayo yanaweza kuwa yanasababisha DKA yako, madaktari wanaweza kufanya vipimo kama vile:

  • Eksirei ya kifua

  • Vipimo vya mkojo

  • ECG (elektrokadiogramu, kipimo kinachopima mikondo ya umeme ya moyo wako na kuzirekodi kwenye karatasi)

Je, madaktari wanatibu vipi DKA?

DKA ni dharura ya kimatibabu. Utahitaji kwenda hospitalini na huenda ukahitaji kulazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).

Madaktari hutibu DKA kwa:

  • Majimaji na elektroliti kwenye mshipa wako wa damu

  • Kuweka Insulini kwenye mshipa wako wa damu

  • Vipimo vya damu kila baada ya saa chache ili kuangalia viwango vya sukari, ketoni na elektroliti ili kuhakikisha kuwa vinarejea katika hali ya kawaida

Madaktari pia hutibu tatizo lingine lolote lililosababisha DKA.