Mizio ya mwaka mzima ni nini?
Mzio hutokea pale ambapo mfumo wa kingamwili humenyuka kutokana na kitu kisicho na madhara, kama vile chakula, mimea, au dawa. Dutu inayosababisha mmenyuko wa mzio huitwa kizio.
Mizio ya mwaka mzima ni:
Mizio ambayo hutokea mwaka mzima
Mizio hii inaweza kutokea katika wakati wowote wa mwaka au mwaka mzima. Hazitokei katika msimu mmoja tu, kama vile mizio ya msimu.
Mizio ya mwaka mzima ni utendanaji wa mwili wako kwa vitu vilivyo hewani, mara nyingi vumbi nyumbani
Kawaida husababisha pua kuziba, kutokwa na kamasi au kuwasha, koo kuwasha, au macho mekundu yanayowasha.
Kuepuka kizio ni bora zaidi, lakini dawa inaweza kutuliza dalili zako
Ni nini husababisha mizio ya mwaka mzima?
Mizio ya mwaka mzima husababishwa na mfumo wa kingamwili kutendana na kitu kisicho na madhara. Mara nyingi husababishwa na:
Vumbi kwenye nyumba
Kinyesi cha mende
Magamba kutoka kwa wanyama vipenzi
Dalili za mzio wa mwaka mzima ni pamoja na?
Dalili zinajumuisha:
Kufungana kwa pua au kuwa na kamasi
Kuwasha kwa pua, mdomo au koo
Macho yenye machozi, wekundu, kuwasha, kuvimba
Kupiga chafya
Matatizo ya kusikia au maambukizi ya mara kwa mara ya masikio (hasa kwa watoto)
Maambukizi ya mara kwa mara ya sanasi au polipu za pua (vivimbe vinavyoota ndani ya pua)
Madaktari hutibu vipi mizio ya mwaka mzima?
Madaktari watakutibu kwa:
Dawa za kupuliza kwenye pua za kotikosteroidi au za kuzibua pua
Antihistamini
Ukipata maambukizi ya mara kwa mara ya sanasi au polipu za pua, madaktari wanaweza:
Fanya upasuaji
Ninawezaje kuzuia dalili kutoka kwa mizio ya mwaka mzima?
Ikiwa una mzio wa vumbi la nyumbani, ondoa au safisha mara kwa mara vitu vinavyokusanya vumbi, kama vile:
Vifaa vidogo, magazeti, na vitabu
Fanicha zilizofunikwa kwa vitambaa
Mapazia na vizuia mwanga vya dirisha
Mazulia
Safisha nyumba yako vizuri:
Pangusa vumbi, tumia kivuta vumbi, na udeki sakafu na nyuso
Osha shuka, foronya na blanketi mara kwa mara kwa maji ya moto
Puliza nyumba yako kwa mvuke wa joto
Angamiza mende
Tumia vitu vinavyosaidia kuzuia vumbi kukusanyika nyumbani kwako, kama vile:
Vitambaa vya magodoro na mito vilivyo na kitambaa kilichofumwa vyema
Mito ya nyuzi za sanisia
Viyoyozi na viondoa unyevunyevu ili kupunguza unyevu hewani
Vivuta hewa na vichungi vya chembechembe vyenye lebo ya HEPA (ufanisi mkubwa)
Ikiwa una mzio wa magamba ya wanyama:
Wazuie wanyama vipenzi wasiingie kwenye vyumba fulani vya nyumba yako
Wanyama, ikijumuisha wanyama vipenzi, wakae nje ya nyumba
Mwoshe mnyama kipenzi wako kila wiki