Angioedema

Imepitiwa/Imerekebishwa Dec 2022

Angioedema ni nini?

Angioedema ni kuvimba kwa uso, midomo, ulimi na koo. Angioedema husababishwa na mmenyuko wa mzio.

  • Uvimbe unaweza kuwa mbaya sana ikawa hata huwezi kupumua

  • Angioedema inaweza kuanza ghafla na kuanza na kuisha kwa wiki au miezi kulingana na chanzo

  • Madaktari wanaweza kukupa epinefrini na antihistamini ili kutuliza dalili zako

Nenda kwenye chumba cha dharura iwapo una uvimbe wa uso au koo.

Angioedema husababishwa na nini?

Angioedema inaweza kuwa utendanaji wa mwili wako na:

  • Dawa, haswa aina fulani ya dawa ya shinikizo la damu inayoitwa kizuizi cha ACE

  • Kuumwa au kung'atwa na wadudu

  • Chanjo za mizio

  • Vyakula, kama vile mayai, samaki, karanga na matunda

Angioedema inaweza kusababishwa na matatizo mengine ya kiafya. Inaweza pia kuwa katika familia yako (angioedema ya kurithi).

Dalili za angioedema ni nini?

Angioedema husababisha uvimbe kwenye uso, midomo na ulimi. Wakati mwingine mdomo na koo lako huvimba kwa ndani, na kuifanya iwe vigumu kumeza au kupumua. Sauti yako inaweza kupwelea.

Pamoja na uvimbe, unaweza pia kuwa na dalili zifuatazo:

  • Mabaka yanayokuja na kutoweka (mabaka mekundu, yanayowasha, yaliyoinuka kwenye ngozi)

  • Maumivu ya tumbo, kutapika, au kukakamaa kwa tumbo

Picha za Angioedema
Angioedema
Angioedema

Picha hii inaonyesha uvimbe midomoni mwa mtu aliye na angioedema ya kurithi.

Kwa idhini ya mchapishaji. Kutoka kwa Joe E, Soter N. In Current Dermatologic Diagnosis and Treatment, ilihaririwa na I Freedberg, IM Freedberg, na MR Sanchez. Philadelphia, Current Medicine, 2001.

Angioedema ya Ulimi
Angioedema ya Ulimi

Mtu huyu ana ulimi uliovimba kutokana na angioedema.

MAKTABA YA PICHA ZA KISAYANSI

Angioedema ya Midomo
Angioedema ya Midomo

Mtu huyu amevimba midomo kutokana na angioedema.

DKT P. MARAZZI/MAKTABA YA PICHA ZA KISAYANSI

Madaktari wanawezaje kujua kama nina angioedema?

Madaktari wanaweza kujua kulingana na dalili zako na kwa kukuchunguza. Ikiwa madaktari hawawezi kubaini chanzo, watakuuliza maswali, ikiwa umeacha kutumia dawa ambazo unaweza kuwa na mzio nazo, na wanaweza kufanya vipimo.

Madaktari hutibu vipi angioedema?

Jambo la muhimu zaidi ni kuweka wazi viungo vyako vya kupumua. Ikiwa unatatizika kupumua, madaktari wanaweza:

  • Kuweka bomba la kupumua kwenye koo lako

  • Kukudunga sindano ya epinefrini

Matibabu mengine hutegemea chanzo ambacho madaktari wanafikiri kilisababisha angioedema yako. Huenda daktari akakupa:

  • Antihistamini za kupunguza kuwashwa na uvimbe

  • Kotikosteroidi

Ikiwa una angioedema ya kurithi, kuna dawa maalum ambazo madaktari wanaweza kukupa kupitia mishipa (IV).

Kuepuka chanzo cha angioedema yako kunaweza kusaidia kuzuia katika siku zijazo. Ikiwa unapata athari kali, unapaswa kubeba dawa za epinefrini na vidonge vya antihistamini kila wakati ili uzitumie ikiwa utaanza kupata athari nyingine. Kisha nenda kwenye chumba cha dharura hospitalini ikiwa unahitaji matibabu zaidi.