Uoni hafifu ni nini?
Uoni hafifu ni wakati hauoni vizuri na dhahiri kama ulivyokuwa unaona mbeleni. Ni tatizo la kawaida zaidi la kuona. Uoni hafifu ni tofauti na kupoteza uwezo wa kuona. Kupoteza uwezo wa kuona inamaanisha kuwa unakuwa kipofu au hauwezi kuona chochote kwa kutumia zote au sehemu ya jicho.
Ni kawaida kwa uwezo wako wa kuona kuwa wenye ukungu polepole unapozeeka, lakini miwani au lenzi za mgusano zinaweza kwa kawaida kukusaidia kuona vizuri
Ikiwa umepoteza uwezo wa kuona kwa ghafla, nenda kwenye hospitali mara moja—kupoteza uwezo wa kuona ni tofauti na uoni hafifu
Nini husababisha uoni hafifu?
Mara nyingi uoni wako ni hafifu na unahitaji tu miwani au lenzi za mgusano kwa sababu wewe ni:
Anayeona karibu vizuri (una tatizo kuona kwa udhahiri vitu vilivyo mbali)
Anayeona mbali vizuri (una tatizo kuona kwa udhahiri vitu vilivyo karibu)
Una astigmati (uoni hafifu kwa sababu ya umbo la konea au lenzi ya jicho lako)
Sababu nyingine za kawaida:
Mtoto wa jicho (wakati lenzi ya jicho lako hupata ukungu polepole)
Kuharibika kwa makyula (kuharibika kwa hatua kwa hatua kwa sehemu ya nyuma ya jicho lako, hivyo kusababisha kupoteza uwezo wa kuona)
Glaukoma (shinikizo la juu ndani ya jicho lako)
Je, napaswa kumwona daktari lini?
Nenda kwenye hospitali mara moja ikiwa una uoni hafifu na una yoyote ya ishara hizi za onyo:
Uoni hafifu wako ulianza kwa ghafla
Kupoteza uwezo wa kuona kali, haswa kwenye jicho moja pekee, hata kama dalili zilianza polepole
Uchungu kwenye macho (ukisongesha au bila kusongesha macho yako)
Kuwa na sehemu za mboni zisizoona—kutoweza kuona sehemu fulani kwenye uwanja wako wa kuona
Una tatizo la mfumo wa kingamwili, kama vile VVU au UKIMWI
Ukiwa una uoni hafifu na matatizo ya afya ambayo yanaweza kusababisha kuharibika kwa jicho, kama vile kisukari, shinikizo la juu la damu, au ugonjwa wa selimundu, nenda kwa daktari wa macho ndani ya siku chache—hata kama hauna ishara za onyo.
Ikiwa una uoni hafifu bila ishara za onyo, kwa kawaida unaweza kusubiri kwa wiki au zaidi ili kwenda kwa daktari wa macho.
Je, nitarajie nini ninapokwenda kumwona daktari wangu?
Daktari atakuuliza kuhusu dalili zako na historia ya afya yako.
Madaktari watafanya:
Kukagua uwezo wako wa kuona kwa kutumia chati ya macho
Kuweka matone ya kioevu kwenye jicho lako (huenda ukahisi mwasho kwa sekunde chache)
Kuangalia ndani ya jicho lako kwa kutumia mwanga maalum wa lenzi (mwangaza mkali sana)
Kupima shinikizo kwenye jicho lako (kuna njia tofauti za kufanya hivyo, lakini hamna inayoumiza)
Je, madaktari wanatibu vipi uoni hafifu?
Madaktari watatibu kisababishaji cha uoni hafifu wako. Kwa mfano, ikiwa una mtoto wa jicho, unaweza kuhitaji upasuaji ili kuitibu.
Madaktari wanaweza kukwambia utumie miwani au lenzi za mgusano ili kukusaidia kuona vizuri zaidi.