Maumivu ya Hedhi

Imepitiwa/Imerekebishwa Nov 2023

Je, maumivu ya hedhi ni nini?

Maumivu ya hedhi ni maumivu kwenye sehemu ya chini ya tumbo ambayo hutokea siku chache kabla, wakati, au baada ya kipindi chako cha hedhi.

  • Maumivu yako yanaweza kuwa ya ghafla au makali

  • Maumivu yanaweza kuanzia sehemu ya chini tumbo hadi sehemu ya chini ya mgongo na chini hadi sehemu ya nyuma ya miguu yako

  • Kupata usingizi wa kutosha, kufanya mazoezi, na kutumia NSAID (dawa za kupunguza maumivu zisizo za steroidi), kama vile ibuprofeni, kunaweza kusaidia kupunguza maumivu yako

Kuna aina 2 za maumivu ya hedhi:

  • Ya kawaida

  • Yasiyo ya kawaida

Maumivu ya kawaida ya hedhi ndiyo aina ya kawaida zaidi. Maumivu kama haya:

  • Kwa kawaida huanza ukiwa kijana

  • Mara nyingi hurithiwa katika familia

  • Kawaida hupungua unapokua au baada ya kupata mtoto

Maumivu ya hedhi yasiyo ya kawaida:

  • Husababishwa na tatizo lingine la kiafya, kama vile fibroidi

  • Kwa kawaida huanza ukiwa mtu mzima

Je, ni nini husababisha maumivu ya hedhi?

Maumivu ya kawaida ya hedhi yanaweza kusababishwa na:

  • Viwango vya juu vya prostaglandini

Prostaglandini ni kemikali ambazo mwili wako hutengeneza. Hufanya uterasi yako kukazika, na miisho ya nyuzi za neva zako kuhisi uchungu zaidi.

Maumivu yasiyo ya kawaida ya hedhi mara nyingi husababishwa na matatizo ya kiafya yanayoathiri uterasi yako kama vile:

  • Endometriosisi: tishu (endometriamu) ambayo kwa kawaida huwa ndani ya uterasi yako hukua nje ya uterasi yako

  • Fibroidi: uvimbe (ambao si saratani) kwenye uterasi yako

  • Adenomiosisi: tishu kwenye utando wa uterasi yako hukua hadi kwenye ukuta wa uterasi yako, na hivyo kuifanya kuwa kubwa na kuvimba wakati wa hedhi

Je, dalili za maumivu ya hedhi ni zipi?

Dalili kuu ni:

  • Maumivu ya ghafla au makali kwenye sehemu ya chini ya tumbo lako—maumivu yanaweza kuja na kupotea, au kuwa na maumivu makali ya mara kwa mara

Huenda pia:

  • Maumivu ya kichwa

  • Kuhisi mgonjwa kwenye tumbo lako au kutapika

  • Kufunga choo

  • Kuhara (kinyesi cha maji, mara kwa mara)

Kuna uwezekano mkubwa wa kuwa na dalili kali ikiwa:

  • Hedhi yako ilianza ukiwa na umri mdogo

  • Unavuja damu kwa wingi kwa muda mrefu wakati wa hedhi

  • Unavuta sigara

  • Una wanafamilia walio na maumivu makali ya hedhi

Je, ni wakati gani ninapaswa kwenda kwa daktari kwa maumivu ya hedhi?

Maumivu ya hedhi hayapendezi lakini si hatari. Hata hivyo, matatizo makubwa zaidi ya afya wakati mwingine husababisha maumivu katika sehemu ya chini ya tumbo.

Nenda kwa daktari leo ikiwa una maumivu katika sehemu ya chini ya tumbo na mojawapo ya haya:

  • Maumivu makali ambayo yalianza ghafla

  • Maumivu ya mara kwa mara

  • Maumivu ambayo yanazidi unapogusa tumbo lako au unapotembea

  • Homa au mzizimo

  • Kutokwa na uchafu mwingi, mweupe au wa manjano (majimaji) kutoka kwenye uke wako

Nenda kwa daktari ndani ya siku chache ikiwa una maumivu ya hedhi ambayo ni mabaya kuliko kawaida au yanayodumu kwa muda mrefu kuliko kawaida. Ikiwa huna maumivu yoyote yaliyo hapo juu, pigia simu daktari wako wakati unaweza.

Je, madaktari wanawezaje kujua ikiwa nina maumivu ya hedhi?

Madaktari watashuku maumivu ya hedhi kulingana na dalili zako na uchunguzi. Ili kuhakikisha kuwa hakuna sababu nyingine ya dalili zako, wanaweza kufanya kipimo kimoja au zaidi:

  • Kupima ujauzito

  • Kipimo cha picha kinachotumia mawimbi ya sauti katika sehumu ya chini ya tumbo lako ili kuchunguza ovari zako, uterasi, na mlango wa kizazi

  • Ikiwa daktari wako anafikiri kuwa unaweza kuwa na ugonjwa wa uvimbe kwenye fupanyonga, atachukua sampuli kutoka kwenye mlango wa kizazi kwa usufi wa pamba na kuipima ili kubaini ikiwa ina maambukizi

Kwa nadra sana, daktari wako anaweza kuhitaji kufanya vipimo vya picha, kama vile MRI (upigaji picha kwa mvumo wa sumaku), au kwa kutumia bomba la kuangalia (histeroskopia) kutazama ndani ya uterasi yako.

Je, madaktari hutibuje maumivu ya hedhi?

Ikiwa una maumivu ya hedhi ya kawaida, madaktari watapendekeza njia za kupunguza maumivu yako:

  • Kupata usingizi wa kutosha

  • Mazoezi

  • Weka pedi ya kupasha joto kwenye sehemu ya chini ya tumo lako

  • Tumia NSAID (dawa za kupunguza maumivu zisizo za steroidi), kama vile ibuprofeni siku moja au 2 kabla ya kuanza kwa kipindi chako cha hedhi na siku 2 za kwanza za kipindi chako cha hedhi

Ikiwa ungali na maumivu, madaktari wanaweza:

  • Kukupa dawa za kuzuia mimba—dawa hizi huzuia ovari zako kutoa yai

  • Kukupa matibabu mengine ya homoni

  • Kujaribu dawa za maumivu ya neva kama vile gabapentini

  • Kupendekeza matibabu mbadala kama vile kudunga ngozi na sindano nyembamba

Ikiwa maumivu yako ni makali sana hata kwa matibabu, madaktari wanaweza:

  • Kufanya upasuaji ili kukata neva zinazotuma ishara za maumivu kutoka kwa uterasi hadi kwa ubongo wako

Ikiwa una maumivu ya hedhi yasiyo ya kawaida, madaktari watatibu tatizo la kiafya linalosababisha maumivu yako.