Kutoa mimba

Imepitiwa/Imerekebishwa May 2023 | Imebadilishwa Jun 2023

Ni nini maana ya kutoa mimba?

Kutoa mimba ni kukomesha ujauzito kwa kutumia dawa au upasuaji.

  • Utoaji mimba ni mojawapo ya aina za upasuaji zinazofanywa sana nchini Marekani

  • Utaratibu wa kutoa mimba ni salama kabisa unapofanywa na daktari aliyehitimu katika kituo cha matibabu

  • Kadiri utaratibu wa kutoa mimba unavyofanywa mapema katika kipindi chako cha ujauzito, ndivyo unavyokuwa rahisi na salama

  • Utaratibu wa kutoa mimba ni hatari unapofanywa na watu ambao hawana ujuzi (kwa mfano katika maeneo ambako kutoa mimba hakujahalalishwa)

  • Unapaswa kuanza kutumia mbinu ya kupanga uzazi punde tu baada ya kutoa mimba

Ni zipi aina za utoaji mimba?

Kuna aina 2 za kutoa mimba:

  • ya upasuaji

  • Za dawa

Katika utoaji mimba wa upasuaji, kijusi hutolewa kwenye uterasi yako kupitia sehemu yako ya uke. Kwa kawaida daktari huweka kifaa cha kuvuta kupitia mlango wa kizazi (uwazi unaoelekeza kwenye uterasi yako). Utoaji mimba wa upasuaji mara nyingi huitwa kupanua na kuondoa (D & E) au kupanua na kukwangua (D & C) kwa kutumia mbinu ya kuvuta.

Katika utoaji mimba wa dawa, daktari hukupa dawa zinazofanya uterasi yako ijibane na isukume kijusi nje.

Mambo gani hufanyika kabla ya kutoa mimba?

Kabla hujatoa mimba, daktari atafanya yafuatayo:

  • Atazungumza nawe na akufanyie uchunguzi ili kubaini iwapo una matatizo yoyote ya kimatibabu

  • Atafafanua utaratibu wa kutoa mimba

  • Atakupa usaidizi wa kisaikolojia kuhusiana na chaguo zingine ulizo nazo za ujauzito wako

  • Atabaini kipindi ulichokaa na ujauzito, kwa kawaida hufanywa kupitia kipimo cha picha kwa kutumia mawimbi ya sauti

  • Fanya vipimo vya damu

Baada ya hatua hizi, huenda ukaweza kutoa mimba mara moja. Hata hivyo, baadhi ya majimbo huhitaji kuwe na kipindi cha kusubiri kati ya ushauri wako nasaha na kutoa mimba. Pia, kwenye utoaji mimba kwa njia ya upasuaji, huenda ukahitaji matibabu kwa siku moja au mbili ili kufungua mlango wa kizazi. Uamuzi wa iwapo unahitaji matibabu haya unategemea kipindi ulichokaa na ujauzito.

Kitu gani hufanyika wakati wa utoaji mimba wa upasuaji?

Utoaji mimba wa upasuaji hufanywa kwenye ofisi au kliniki.

Kabla ya kuanza, daktari atafanya yafuatayo:

  • Atakupa dawa za kumeza kwa kinywa za kuua bakteria ili kuzuia maambukizi

  • Atakupa matibabu ya kufungua mlango wa kizazi, isipokuwa kama mimba yako ni changa mno

Mchakato wa kufungua mlango wako wa kizazi unaitwa upanuaji. Ili kufungua mlango wa kizazi, daktari wako anaweza:

  • Kukupa dawa kwa kinywa au kupitia uke wako

  • Kuweka kipande kidogo kwenye mlango wa kizazi

Kitu anachoweka daktari kwenye mlango wa kizazi hufyonza maji na kuvimba ili kufungua mlango wa kizazi. Wakati mwingine hatua hii hukamilika baada ya saa kadhaa, lakini inaweza kuchukua siku moja au mbili.

Kwenye utoaji mimba wa upasuaji, daktari atafanya yafuatayo:

  • Atakupa dawa kupitia kwenye mshipa ya kukufanya ulale ili usihisi upasuaji unapofanyika

  • Atadunga dawa ya ganzi ndani ya uke wako karibu na mlango wako wa kizazi.

  • Ataweka tyubu ndogo inayoweza kupinda kupitia mlango wako wa kizazi hadi ndani ya uterasi ili kuondoa kilichomo na kutamatisha ujauzito wako

  • Wakati mwingine atakwangua sehemu ya ndani ya uterasi yako ili kuhakikisha kuwa kilichomo kimetoka

Ni kitu gani hufanyika wakati wa utoaji mimba wa dawa?

Utoaji mmba wa dawa (tembe) kwa kawaida hufanywa katika wili za kwanza 9 hadi 11 za ujauzito. Baadaye katika ujauzito, utoaji mimba huwa changamano zaidi na hulazimu kufanywa kwa mbinu ya upasuaji.

Kwenye utoaji mimba wa dawa kabla ujauzito haujafikisha wiki 9 hadi 11, kwa kawaida utafanya yafuatayo:

  • Utameza dawa kwa kinywa

  • Utakunya dawa nyingine baada ya siku moja au mbili

Dawa hiyo hufanya uterasi yako ikaze (ijibane). Tumbo lako litasokota, utapata hisia ya kichefuchefu tumboni, na kutokwa na damu kupitia uke wako wakati kilichomo kwenye uterasi yako kinatoka. Kwa kawaida, ujauzito wako hukomeshwa ndani ya saa 24 hadi 48 baada ya kumeza dawa hii.

Je, kutoa mimba ni salama kiasi gani?

Utoaji mimba ambao ni halali kisheria unaofanywa na madaktari kwenye vituo vya matibabu ni salama sana. Pia, kutoa mimba hakuongezi uwezekano wako wa kupata matatizo ya ujauzito katika siku za usoni.

Wanawake wengi hupata matatizo kutokana na kujifungua mtoto kuliko kutoa mimba. Hata hivyo, unapaswa kukumbuka kuwa kutumia mbinu za kupanga uzazi kuzuia ujauzito ni salama zaidi kuliko kutoa mimba.

Matatizo makubwa yanapotokana na kutoa mimba, huwa yanatokea katika wiki ya kwanza baada ya kutoa mimba. Uwezekano wa kupata matatizo unaongezeka kadiri muda wa ujauzito wako ulivyosonga wakati wa kutoa mimba. Matatizo makubwa ni pamoja na:

  • Kupata tundu kwenye uterasi au kuchanika kwenye mlango wako wa kizazi kutokana na vifaa vya kutoa mimba

  • Kuvuja damu sana

  • Maambukizi kwenye uterasi yako

Unapaswa kurudi kwa daktari wako iwapo una:

  • Homa

  • Kuvuja damu sana

  • Maumivu kwenye tumbo lako (zaidi ya maumivu ya kawaida ya mkakamao wa misuli)

Ili kusaidia kuzuia maambukizi, hupaswi kujamiiana kwa wiki 2 baada ya kutoa mimba.