Kisonono ni nini?
Kisonono ni maambukizi ya zinaa (STI). Ugonjwa wa zinaa ni maambukizi ambayo huenezwa kutoka kwa mtu hadi mwingine kupitia ngono. Kisonono huambukiza sehemu zako za siri na, kwa wanawake, mirija ya uzazi na ovari. Mirija ya uzazi huunganisha ovari zako (mahali mayai yako yanapohifadhiwa) na uterasi yako.
Wakati mwingine, ngono ya kinywa inaweza kusababisha maambukizi ya kisonono kwenye koo. Ngono kwa njia ya haja kubwa inaweza kusababisha maambukizi ya kisonono kwenye rektamu yako (pale ambapo kinyesi huhifadhiwa).
Unaweza kupata kisonono kwa kushiriki ngono ya uke, mdomo, au kwa tundu la haja kubwa na mtu aliyeambukizwa
Mwanamke mjamzito anaweza kuambukiza macho ya mtoto wake kisonono wakati wa kuzaliwa
Kisonono husababisha dalili kwenye sehemu yako ya mwili iliyoambukizwa, lakini inaweza kuenezwa kwa sehemu nyingine za mwili wako, kama vile viungo au ngozi.
Ikiwa unashiriki ngono au ni mjamzito, zungumza na daktari wako kuhusu kipimo cha uchunguzi wa kisonono
Madaktari hutibu kisonono kwa dawa za kuua bakteria
Mwanamke ambaye ana kisonono akikosa kutibiwa anaweza kupata ugonjwa wa kuchochewa kwa fupanyonga (PID). PID ni maambukizi kwenye uterasi, mirija ya uzazi au zote mbili. PID pia inaweza kusambaa katika ovari zako na kwenye mtiririko wa damu. PID inaweza kuharibu viungo vyako vya uzazi na kufanya iwe vigumu kupata mtoto.
Mwanamume ambaye ana kisonono anaweza pia kupata epididimitisi, maambukizi ya epididimisi. Epididimisi ni bomba lililojikunja sehemu ya juu ya korodani. Ugonjwa wa epididimitisi husababisha maumivu na uvimbe ya mfuko wako wa korodani.
Je, dalili za kisonono ni zipi?
Wanawake
Maumivu kwenye sehemu ya uke
Majimaji ya manjano kutoka kwenye uke wako (vitu kutoka ukeni)
Kuhisi kama unahitaji kukojoa (haja ndogo) zaidi kuliko kawaida
Maumivu unapokojoa
Maumivu makali katika tumbo lako la chini ukipata uvimbe kwenye fupanyonga
Wanaume
Maumivu madogo hadi makali unapokojoa
Uchafu wa manjano-kijani (majimaji mazito) kutoka kwenye uume
Kuhisi kukojoa zaidi kuliko kawaida
Mdomo wa kwa uume wako kuwa mwekundu
Uvimbe wenye maumivu kwenye korodani kwa pande moja au zote mbili ikiwa una epididimitisi
Wanawake na wanaume
Ikiwa rektamu (pale ambapo kinyesi huhifadhiwa) au tundu la haja kubwa (sehemu kinyesi kinapotoka) limeambukizwa, unaweza kupata maumivu na kutokwa na uchafu mzito wa manjano kutoka kwenye tundu lako la haja kubwa.
Ikiwa koo lako limeambukizwa, kwa kawaida hutakuwa na dalili yoyote, lakini unaweza kuhisi mkwaruzo kwenye koo.
Madaktari wanawezaje kujua kuwa nina kisonono?
Madaktari hushuku kisonono kulingana na dalili zako.
Ili kuhakikisha, watapima sampuli kutoka kwa uume, uke, koo au rektamu yako.
Huenda daktari wako akapitisha pamba ndogo kwenye uume, koo, au rektamu yako ili kupata sampuli ya majimaji ya kupima. Ikiwa wewe ni mwanamke, daktari wako ataangalia kwenye uke wako kwa kutumia spekulamu ya plastiki na kuchukua vitu vinavyotoka kwenye mlango wako wa kizazi (sehemu ya chini ya tumbo lako la uzazi iliyowazi hadi kwenye uke wako).
Ikiwa wewe ni mjamzito au uko katika hatari kubwa ya kuwa na kisonono, daktari wako anaweza kufanya kipimo cha mkojo cha kisonono iwapo huna dalili zozote. Wanawake wako katika hatari kubwa zaidi kwa:
Kushiriki ngono wakiwa chini ya miaka 25
Umewahi kuwa na ugonjwa wa zinaa
Kushiriki katika shughuli hatari za ngono (kama vile kushiriki katika biashara ya ngono, kuwa na mwenzi anayefanya biashara ya ngono, kuwa na wapenzi wengi, au kutotumia kondomu mara kwa mara)
Kuwa na mpenzi anayefanya shughuli hatari za ngono
Wanaume wako katika hatari kubwa zaidi kwa:
Kushiriki ngono na mwanaume mwenzao ndani ya mwaka mmoja uliopita
Huenda daktari akakupima pia damu au mkojo wako kuchunguza magonjwa mengine ya zinaa kwa sababu watu wengi wana zaidi ya ugonjwa mmoja wa zinaa.
Madaktari hutibu vipi kisonono?
Madaktari watafanya:
Watakuchoma sindano ya dawa za kuua bakteria kwenye misuli
Watakupa dawa za kuua bakteria za kumeza
Watakuambia uepuke kushiriki ngono hadi umalize dawa zako zote za kuua bakteria ili kuzuia kueneza kisonono
Watakutibu hospitalini kwa dawa za kuua bakteria kupitia mshipa (IV) ikiwa maambukizi yalisambaa kwenye viungo vyako
Watampima na kumtibu mwenzi wako wa ngono kisonono