Saratani ya tezi dundumio

Imepitiwa/Imerekebishwa Jun 2024

Dundumio yako inapatikana chini ya kongomeo kwenye shingo yako.

Dundumio lako hutengeneza homoni za dundumio. Homoni hudhibiti kasi ya utendakazi wa kemikali za mwili wako (kiwango cha kimetaboli). Karibu kila seli mwilini inahitaji homoni za dundumio. Miongoni mwa majukumu mengine mengi, homoni za dundumio husaidia kudhibiti:

  • Jinsi mwili unavyotumia kalori

  • Jinsi moyo wako unavyopiga haraka

  • Joto la mwili wako

Kufikia Tezi Dundumio

Saratani ya tezi dundumio ni nini?

Saratani ya tezi dundumio ni saratani ambayo iko kwenye dundumio lako.

  • Hatua ya kwanza ya saratani ya tezi dundumio kwa kawaida ni uvimbe usio na maumivu kwenye shingo lako

  • Kuna aina 4 kuu za saratani ya tezi dundumio

  • Saratani ya tezi dundumio inapatikana sana kwa wanawake na watu waliotibiwa kwa mionzi wakiwa watoto

  • Madaktari wanatibu aina tofuati za saratani ya tezi dundumio kwa njia tofauti

  • Aina ya kawaida sana ya saratani ya tezi dundumio mara nyingi inatibika

Zipi ni aina za saratani ya tezi dundumio?

Kuna aina 4 za saratani ya tezi dundumio:

  • Papilari (ambayo inapatikana kwa wingi na rahisi kutibika).

  • Folikyula

  • Medulari

  • Anaplastiki (nadra sana lakini ya hatari zaidi)

Nini kinasababisha saratani ya tezi dundumio?

Madaktari hawajui kinachosababisha saratani ya tezi dundumio. Inapatikana sana kwa wanawake na watu waliotibiwa kwa mionzi kwenye kichwa, shingo au kifua wakiwa watoto. Baadhi ya aina za saratani ya tezi dundumio zisizo patikana sana huwa za kurithi katika familia.

Zipi ni dalili za saratani ya tezi dundumio?

Uvimbe usio na maumivu kwenye shingo lako kwa kawaida ni hatua ya kwanza ya saratani ya tezi dundumio.

Wakati mwingine saratani kubwa inaweza kukandamiza shingo lako, na kusababisha:

  • Kuhisi umevimba shingo

  • Sauti yenye kukwaruza

  • Kikohozi

  • Ugumu wa kupumua

Saratani ya tezi dundumio kwa kawaida huwa haitengenezi homoni za dundumio kwa hivyo huna uwezekano wa kuwa na dalili za hipathiroidi (homoni nyingi sana za dundumio).

Madaktari wanawezaje kujua kuwa nina saratani ya tezi dundumio?

Madaktari baada ya kuona uvimbe kwenye shingo lako, wanaweza kufanya:

  • Vipimo vya damu ili kupima kazi ya dundumio

  • Kipimo cha picha kwa kutumia mawimbi ya sauti

  • Uondoaji wa kipande cha tishu kwa uchunguzi (sampuli ya uvimbe inayochukuliwa kwa sindano ndogo na kuchunguzwa kwenye hadubini)

Je, madaktari wanatibu vipi saratani ya tezi dundumio?

Matibabu yanategemea aina ya saratani na iwapo imesambaa, lakini madaktari mara nyingi:

  • Wanafanya upasuaji ili kuondoa sehemu au tezi dundumio yako yote

Baada ya upasuaji, unaweza kupata iodini ya mionzi au tiba ya mionzi ili kuondokana na saratani yoyote iliyosalia.

Baada ya matibabu, utakuwa na kazi ndogo za dundumio au zisiwepo kabisa, kwa hivyo utapaswa kuchukua:

  • Vidonge vya homoni za dundumio