Usonji ni nini?

Usonji ni tatizo la ubongo ambalo linaathiri jinsi watu wanavyoingiliana na watu wengine na kuwasiliana.

Watu wenye utonji wanapata shida ya kuzungumza na kuhusiana na watu wengine. Pia wana tabia zisizo za kawaida. Neno usonji linarejelea wigo wote (spektra) wa matatizo yanayohusiana. Kwa hivyo madaktari wanayaita haya ugonjwa wa spektra wa usonji.

  • Watoto wenye usonji kwa kawaida wana tabia zisizo za kawaida, za kujirudia, wana mapendeleo machache na wanafuata kaida zisizobadilika

  • Usonji unaanza utotoni na kwa kawaida unaonekana kabla ya miaka 2

  • Watoto wenye dalili zisizo kali wanaweza wasitambulike hadi wafikie umri wa kwenda shule

  • Usonji ni tofuati na kuwa na uwezo mdogo wa akili (ulemavu wa akili)

  • Usonji hausababishwi na chanjo au malezi mabaya

Je, dalili za usonji ni zipi?

Watoto wenye usonji wana dalili tofauti mbalimbali. Na ukali wa dalili hutofautiana. Hata hivyo, dalili tofuati kwa kawaida zinahusisha mambo mawili:

  • Kupata shida kuwasiliana na kuingiliana na watu

  • Tabia, mapendeleo au shuguli zisizo za kawaida za kujirudia

Dalili hizi zinaanza katika umri mdogo, mara nyingi wakati mtoto wako bado mchanga. Hata hivyo, wewe na daktari wako mnaweza kutambua dalili hizi pale tu mtakapoangalia nyuma.

Kwa watoto wachanga, shida ya mawasiliano hujumisha:

  • Kutobwabwaja

  • Kutoakutanisha macho

Kwa watoto wadogo, shida ya kuwasiliana na kuingiliana hujumuisha:

  • Kuwa mzito kuanza kuzungumza au kutojifunza kabisa kuzungumza

  • Kuepuka kukutanisha macho anapozungumza na mtu

  • Kurudia maneno ambayo watu wengine wamezungumza

  • Kuzungumza kwa mtindo usio wa kawaida

  • Kushindwa kuelewa ikiwa mtu ana furaha, hasira au huzuni kutokana na sura yake au lugha ya mwili

  • Kutoshiriki mawazo na hisia zao pamoja na wengine

  • Kutokuwa na shauku ya kuwa na marafiki

  • Kuchagua kucheza peke yao

Dalili za tabia na shughuli hujumuisha:

  • Kukasirishwa sana na mabadiliko yoyote, kama vile chakula kipya, vitu vya kuchezea na nguo

  • Kukerwa sana na ladha fulani, harufu au maumbile

  • Kutikisa, kupigapiga mikono a kuzunguka

  • Kugonga kichwa au kujing'ata wenyewe

  • Kurudia vitendo fulani, kama vile kutazama filamu ile ile tene na tena au kula chakula kile kile katika kila mlo

  • Mapendeleo yasiyo ya kawaida, kwa mfano kuvutiwa sana na vinyonya vumbi au feni

Watu wengi wenye usonji pia wana ulemavu wa akili na tatizo la kujifunza. Kwa kawaida, alama zinakuwa chini kwenye majaribio ya kuzungumza kuliko maeneo mengine.

Madaktari wanawezaje kujua ikiwa mtoto wangu ana usonji?

Madaktari watamwangalia mtoto wako kwenye chumba cha michezo na kukuuliza wewe na walimu wa mtoto wako maswali. Kwa kawaida watampeleka mtoto wako kwa mtaalamu wa saikolojia kwa ajili ya vipimo vingine.

Madaktari pia watafanya vipimo vya damu au jenetiki kuangalia ikiwa kuna tatizo tofuati linalosababisha dalili za mtoto wako, kama vile matatizo ya kijenetiki (tatizo la kiafya la kurithi).

Usonji unatibiwa vipi?

Kwa kawaida dalili ni za kudumu. Watu wenye usonji wanaopata alama za chini za akili wana uwezekano wa kupata usaidizi zaidi katika maisha yao wanapokuwa watu wazima.

Usonji unatibiwa kwa kutumia:

  • Tiba ya tabia ili kutengeneza ujuzi wa kijamii

  • Elimu maalumu shuleni

  • Wakati mwingine dawa, kama vile vizuizi vya uchaguzi wa kuchukua tena serotonini (SSRI) au dawa nyinginezo ambazo zinaweza kusaidia waache kujiumiza

Baadhi ya familia wanajaribu mlo maalumu au tiba mbadala. Hakuna ushahidi mzuri kwamba njia hizi zinasaidia watoto wenye usonji. Zungumza na daktari wako kuhusu tiba zozote unazozifikiria.