Kiwewe Sugu cha Ubongo (CTE)

(Pugilistika ya Kupungua kwa Utambuzi)

Imepitiwa/Imerekebishwa Dec 2022

Je, kiwewe sugu cha ubongo (CTE) ni nini?

Ugonjwa wa kiwewe sugu cha ubongo (CTE) ni kuharibika kwa seli za ubongo kwa kipindi cha muda mrefu. Unasababishwa na majeraha ya mara kwa mara kichwani au sauti za milipuko. Majeraha ya kichwa ni pamoja na jeraha la ubongo linalotokana na kupigwa/kugongwa.

  • Madaktari hawana uhakika kuhusu sababu ya baadhi ya watu walio na majeraha ya kichwa hupata Kiwewe Sugu cha Ubongo na wengine hawapati

  • Dalili za Kiwewe Sugu cha Ubongo zinaweza kujumuisha unyogovu, hasira, kuchanganyikiwa, mabadiliko ya haiba na matatizo ya kutembea haraka au kuzungumza kwa uwazi

  • Hakuna tiba ya Kiwewe Sugu cha Ubongo

  • Matibabu husaidia kuboresha dalili za hisia na kuhakikisha kuwa mtu anahisi vizuri na salama

Kiwewe sugu cha ubongo (CTE) ni aina ya hali ya kupungua kwa utambuzi, ambayo ni tatizo la ubongo linalofanya iwe vigumu kukumbuka, kufikiri na kujifunza.

Je, Kiwewe Sugu cha Ubongo husababishwa na nini?

Kiwewe Sugu cha Ubongo husababishwa na:

  • Majeraha ya mara kwa mara ya kichwa, kama vile kuotokana na kucheza mpira wa miguu, ndondi, au michezo mingine—kila jeraha la kichwa halihitaji kuwa kali ili kusababisha Kiwewe sugu cha ubongo

  • Majeraha ya kichwa kutokana na mlipuko, mara nyingi hutokea kwa wanajeshi katika mapigano

Je, dalili za Kiwewe sugu cha ubongo ni zipi?

Dalili za Kiwewe sugu cha ubongo huenda zisiwepo hadi baadaye maishani, wakati mwingine hadi baada ya miaka 60.

Baadhi ya watu wenye Kiwewe sugu cha ubongo wana dalili dhaifu wanapokuwa vijana wadogo ambazo huwa mbaya zaidi kadri wanavyozeeka.

Dalili zinajumuisha:

  • Mfadhaiko

  • Kukasirika ovyo

  • Mawazo ya kujiua

  • Kuwa na hasira

  • Kupoteza hasira kwa haraka.

  • Kupungua kwa utambuzi

  • Matatizo katika kupanga au kuratibu

  • Kufanya mambo bila welevu

  • Kuwa na shida ya kuzungumza kwa usahihi

Je, madaktari wanawezaje kujua ikiwa nina Kiwewe Sugu cha Ubongo?

Madaktari wanashuku kuwa Kiwewe Sugu cha Ubongo kwa watu ambao wamekuwa na matukio mengi ya majeraha ya kichwa au kuwa kwenye sehemu zilizo na milipuko mikubwa na wana dalili za Kiwewe Sugu cha Ubongo.

Hakuna kipimo cha kuthibitisha utambuzi wa Kiwewe Sugu cha Ubongo, lakini madaktari watafanya vipimo vya picha ya ubongo kama vile uchunguzi wa picha ya (tomografia ya kompyuta). Vipimo vya picha huwasaidia madaktari kuona ikiwa mtu ana hali nyingine yenye dalili sawa. Njia pekee ya madaktari kujua kwa uhakika kuwa mtu ana Kiwewe Sugu cha Ubongo ni kwa kuchunguza ubongo wa mtu baada ya kifo.

Je, madaktari hutibu vipi Kiwewe Sugu cha Ubongo?

Hakuna tiba ya Kiwewe Sugu cha Ubongo, lakini mambo yafuatayo husaidia:

  • Kuishi katika mazingira salama yaliyo na ratiba na shughuli za kawaida

  • Kuelezea kwa uwazi mabadiliko yoyote katika mazingira au watunzaji

  • Usaidizi wa kisaikolojia

  • Kutumia dawa za kusaidia kukabiliana na dalili

Ili kusaidia kupunguza hatari ya kupata Kiwewe Sugu cha Ubongo, watu ambao wamewahi kupata jeraha la ubongo linalotokana na kupigwa/kugongwa wanapaswa kupumzika na kukaa mbali na shughuli za riadha kwa muda.

Kabla ya uwezo wao wa kufanya uamuzi kuathiriwa, watu walio na Kiwewe Sugu cha Ubongo wanapaswa kufanya maamuzi mengi ya matibabu, kifedha na kisheria iwezekanavyo. Hii ni pamoja na kuchagua mtu ambaye anaweza kufanya maamuzi ya ziada ya matibabu kwa niaba yako pindi tu unaposhindwa kufanya hivyo. Unapaswa pia kujadiliana na daktari wako aina ya huduma utakayotaka mwishoni mwa maisha yako (wosia wa kuishi).

Ugonjwa wa Kiwewe Sugu cha Ubongo unapozidi, matibabu huwa kwa ajili ya faraja badala ya kuongeza muda wa kuishi.

Kuwashughulikia walezi

Kuwahudumia watu walio na aina yoyote ya tatizo la kupungua kwa utambuzi, ikiwa ni pamoja na ugonjwa wa kiwewe sugu cha ubongo (CTE), ni kazi inayochosha na yenye mahitaji mengi. Huenda walezi wakafadhaika na kuchoka, na mara nyingi kutoshughulikia afya ya mwili na akili. Ni muhimu kwa walezi:

  • Kujifunza jinsi ya kukidhi mahitaji ya watu wenye tatizo la kupungua kwa utambuzi na cha kutarajia kutoka kwao

  • Kutafuta usaidizi inapohitajika, kama vile utunzaji wa mchana, kutembelewa na wauguzi nyumbani, usaidizi wa kutunza nyumba, usaidizi kutoka kwa mtu unayeishi naye, ushauri nasaha na vikundi vya kusaidiana

  • Kujitengea muda, ikiwemo kutangamana na marafiki na kufanya mambo yanayowavutia na shughuli wanazofurahia