Kujifungua Kwa Njia ya Upasuaji (upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi)

Imepitiwa/Imerekebishwa Sept 2023

Kujifungua kwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi ni nini?

Kujifungua kwa njia ya upasuaji ni upasuaji wa kumzaa mtoto wako kupitia kukatwa kwenye tumbo lako na uterasi.

Kujifungua Kwa Njia ya Upasuaji
Ficha Maelezo
Kwa uzalishaji wa njia ya upasuaji, tumbo na uterasi hukatwa. Mkato huu mara nyingi ni wa mlalo kwenye sehemu ya chini ya uterasi.

Kwa nini nitajitaji kufanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi?

Unaweza kuhitaji kufanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi ikiwa daktari anaona inaweza kuwa salama zaidi kwako au mtoto wako kuliko kujifungua kwa njia ya kawaida ya uke, kama vile wakati ambapo:

  • Uchungu wako unadumu kwa muda mrefu

  • Mtoto wako yupo katika mkao usio wa kawaida, kama vile kuwa kinyumenyume (kutanguliza matako)

  • Mtoto wako yupo katika hatari (shida ya fetasi) na anataiwa kuzaliwa haraka sana

  • Unavuja damu sana

  • Ulijifungua kwa njia ya upasuaji hapo kabla

Je, ninaweza kujifungua mtoto kwa njia ya kawaida ikiwa nilifanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi hapo kabla?

Unaweza kujifungua mtoto wako kawaida kwa njia ya uke ikiwa ulifanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi mara moja tu hapo kabla na mkato ulikuwa katika sehemu ya chini ya uterasi. Ikiwa uliwahi kufanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi zaidi ya mara moja, madaktari wengi watataka ufanyiwe upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi ukiwa na ujauzito mwingine. Daktari wako atakusaidia kuamua ni aina gani ya kujifungua ambayo ni salama zaidi kwako na kwa mtoto wako.

Kitu gani hufanyika wakati wa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi?

Watu kadhaa wanaweza kuwa chumbani unapofanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi, ikiwa ni pamoja na:

  • Daktari wa masuala ya ujauzito, kujifungua na watoto wachanga (daktari anayewahudumia wanawake wajawazito na kuwasaidia kujifungua watoto)

  • Mtaalam wa ganzi/nusukaputi (daktari ambaye anakupa dawa za maumivu na anakufanya ulale kwa ajili ya upasuaji)

  • Wakati mwingine daktari wa watoto (daktari anayewahudumia watoto wachanga na watoto wakubwa)

  • Wauguzi

Madaktari watakupa dawa ili usihisi maumivu wakati wa upasuaji. Kwa kawaida watadunga dawa ya ganzi mgongoni mwako. Dawa ya ganzi inakufanya usihisi maumivu chini ya kiuno chako.

Daktari atamwondoa mtoto wako kupitia upasuaji kwenye tumbo lako na uterasi. Mchano unaweza kuwa katika sehemu ya chini au ya juu ya uterasi wako:

Mkato wa chini: Hii hutokea sana. Husababisha kuvuja damu kidogo na kwa kawaida hupona vizuri.

Mkato wa juu: Madaktari wanatumia njia hii wakati tu wanapolazimika kufanya hivyo, kama vile wakati ambapo:

  • Una hali ya kondo kujipachika upande wa chini (wakati ambapo kondo limejipachika kwenye sehemu isiyo sahihi kwenye uterasi yako)

  • Mtoto wako amekaa pembeni kwenye uterasi yako

  • Mtoto wako amezaliwa mapema sana

  • Mtoto wako ana kasoro ya kuzaliwa

Madaktari watashona uterasi yako na kufunga tumbo. Utapata dawa za kuua bakteria na kuongezewa damu ili kufidia damu uliyopoteza, ikiwa unaihitaji.

Daktari wako atakuruhusu utembee muda mfupi baada ya kufanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi. Kutembea kunasaidia kufanya damu isigande kwenye miguu yako au pelvis. Kuganda kwa damu kunakotokea kwenye miguu yako inaweza kusafiri hadi kwenye mapafu na kusababisha matatizo makubwa.

Je, kufanyiwa upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi ni salama kiasi gani?

Dawa na kuongezewa damu husaidia kufanya upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi kuwa salama. Ukilinganisha na kuzaa kwa njia ya kawaida, upasuaji wa kupasua tumbo la uzazi husababisha:

  • Maumivu zaidi baada ya kujifungua

  • Kukaa hospitalini kwa muda mrefu zaidi

  • Muda mrefu zaidi wa kupona