Je, kunguni ni nini?

Kunguni ni wadudu wadogo wasio na manyoya ambao wanajificha kwenye nyufa za magodoro na kwenye mbao za kitanda, makusheni na kuta. Wanakula damu ya watu na baadhi ya wanyama.

  • Kunguni wanajificha wakati wa mchana kwa hivyo unaweza usiwaone kabisa

  • Wanatoka nje usiku na kukuuma unapokuwa umelala

  • Uumaji wa kunguni hauwezi kukuamsha, lakini utakuwa na alama ya kuumwa nyekundu, inayowasha wakati wa asubuhi

  • Unaweza kuona alama ndogo za damu au alama nyeusi kwenye mashuka yako au godoro

  • Unaweza kuhisi usumbufu mkubwa unapokuwa na kunguni, lakini hawaenezi ugonjwa

  • Ni vigumu sana kuwaondoa kunguni lakini kiangamizi kinaweza kusaidia

Ikiwa utakaa usiku mzima kwenye sehemu yenye kunguni, wadudu hao wanawea kuingia kwenye begi lako la nguo. Kisha unaweza kwenda na kunguni sehemu unapokwenda, ikiwa ni pamoja na nyumbani kwako.

Alama ya kuumwa na kunguni inaonekanaje?

Alama za kuumwa na kunguni kwa kawaida zinaonekana kwenye ngozi yako wakati wa asubuhi, lakini zinaweza zisionekane kwa siku kadhaa. Unaweza kuwa na alama kadhaa za kuumwa katika msitari ulionyooka au katika makundi.

Alama za kuumwa kwa kawaida:

  • Zinakuwa nyekundu, zimevimba, uvimbe unaowasha

Alama za kuumwa pia zinaweza kuonekana kama:

  • Vishimo vidogo

  • Madoa bapa ya zambarau

  • Malengelenge

Alama za kuumwa zinaondoka baada ya karibu wiki moja. Ikiwa utakuna sehemu ulipoumwa, unaweza kupata maambukizi.

Daktari wangu atajua vipi kuwa nimeumwa na kunguni?

Madaktari watashuku kuwa na alama za kuumwa na kunguni ikiwa utaamka ukakuta una uvimbe unaowasha kwenye maeneo ambayo yamefunikwa na mashuka yako. Uthibitisho thabiti ni kuona madoa ya damu kwenye mashuka yako. Anaweza kukuambia ukague magodoro yako na kwenye nyufa za mkunjo wa mbao mahali ambapo kuta zako zinakutana na sakafu. Unaweza kuona vinyesi vya wadudu hao au wadudu wenyewe. Alama za kuumwa na kunguni zinaweza kuwa vigumu kuzitofautisha na alama za kuumwa na wadudu wengine.

Madaktari wanatibu vipi alama za kuumwa na kunguni?

Madaktari wanatibu mwasho unatokana na kuumwa na wadudu kwa kutumia:

  • Krimu ya kotikosteroidi

  • Dawa ya antihistamini

Je, nitawezaje kuondokana na kunguni?

Ni bora zaidi kupata usaidizi wa muuangamiza wadudu mweledi. Wataalamu wanaweza kupendekeza:

  • Kuvuta vumbi kwenye maeneo yenye wadudu wengi

  • Kufua nguo na mashuka, kisha kuzikausha kwa joto kali kabisa

  • Kupasha joto chumba chote kwa hali joto la zaidi ya 122° F (50° C)

  • Viuatilifu (kemikali za kuua wadudu)

Kunguni mara nyingi hawafi kwa urahisi kwa kutumia viuatilifu (dawa ya kunyunyizia wadudu).

Je, ninawezaje kuzuia kunguni?

Unapokaa kwenye hoteli au kwenye nyumba ya mtu mwingine, funga begi lako la nguo na usiliweke kwenye sakafu. Kunguni wanapenda kuingia kwenye mabegi yaliyo kwenye sakafu.