Bulimia Nervosa

Imepitiwa/Imerekebishwa Jan 2024

Je, bulimia ni nini?

Bulimia ni tatizo la kula ambapo:

  • Unakula chakula kingi kwa wakati mmoja (kula kupita kiasi)

  • Kisha fanya mambo ya kurekebisha hali ya kula kupita kiasi (kusafisha tumbo)

Ili kurekebisha kula kupita kiasi, watu wengi hujitapisha na kufanya mazoezi sana. Hata hivyo, baadhi ya watu hutumia dawa za kuwasaidia kwenda haja kubwa ya kuendesha. Au wanaweza kunywa tembe za maji (Dawa zinazosaidia kupunguza mkusanyiko wa maji mwilini) ili kukojoa. Kwa kawaida, huishia kuwa na uzani wa karibu na wa wastani.

Bulimia kwa kawaida huanza katika miaka ya ujana au miaka ya mwanzo wa utu uzima na hutokea zaidi kwa wasichana na wanawake. Inaweza kusababishwa na shinikizo za kijamii kuwa mwembamba. Bulimia inaweza kutokea katika familia yako.

Je, dalili za bulimia ni zipi?

Dalili kuu ni kula mara kwa mara kupita kiasi na kujisafisha.

Unapokula kupita kiasi, unaweza:

  • Kula chakula kingi zaidi kwa wakati mmoja kuliko watu wengi, wakati mwingine mara kadhaa kwa siku

  • Kula wakati hauna njaa

  • Kula sana hadi unapata maumivu ya tumbo

  • Kula kwa siri na kuhisi kuwa huwezi kudhibiti ulaji wako

  • Mara nyingi kula vyakula vitamu, vyenye mafuta mengi (kama keki na aiskrimu)

  • Kuhisi kuwa na hatia sana kutokana na kula sana

Baada ya kula kupita kiasi, unaweza kusafisha tumbo ili kurekebisha hali ya kuwa umekula sana, kwa hivyo unaweza:

  • Kujilazimisha kutapika

  • Kumeza dawa za kutibu tatizo la kufunga choo ili uweze kupata haja kubwa (kinyesi)

  • Kutokula kabisa (kufunga) au kujinyima chakula kupita kiasi

  • Kufanya mazoezi kupita kiasi

Unazingatia uzani na umbo la mwili wako zaidi kuliko unavyopaswa. Mara nyingi unahisi vibaya jinsi mwili wako unavyoonekana hata kama watu wengine wanafikiri kuwa unaonekana sawa.

Tofauti na matatizo mengine ya kula, watu wenye bulimia mara nyingi huwa na uzani wa wastani. Lakini uzani wao unaweza kupanda au kushuka kuliko kawaida.

Je, bulimia inaweza kusababisha matatizo mengine?

Ndiyo. Kujitapisha ili kufidia kula kupita kiasi kunaweza kuumiza mwili wako. Ikiwa utasafisha tumbo sana, unaweza kuwa mgonjwa na hata kuaga dunia. Kujitapisha sana kunaweza kusababisha:

  • Makovu kwenye vifundo vyako kutokana na kuweka vidole vyako kwenye koo ili kujilazimisha kutapika

  • Uharibifu wa meno yako kutokana na asidi ya tumbo

  • Kuvimba kwa tezi kwenye mashavu yako

  • Uharibifu wa umio wako (mrija unaounganisha mdomo wako na tumbo lako) kutoka kwa asidi ya tumbo

  • Kwa nadra, kuchanika kwa tumbo au umio, hali ambayo inaweza kutishia maisha

Kutumia dawa nyingi za kutibu tatizo la kufunga kwa choo au tembe za maji na kutapika sana kunaweza kuharibu usawa wa kemikali katika mwili wako. Usawasisho usio wa kawaida wa kemikali unaweza kuathiri vibaya kupiga kwa moyo wako.

Je, madaktari wanawezaje kubaini kuwa nina bulimia?

Madaktari hufanya vipimo vya kimwili ili kuangalia dalili za bulimia. Madaktari watagundua bulimia ikiwa:

  • Unaweka picha yako ya kibinafsi kwa kiasi kikubwa juu ya uzani na umbo lako

  • Kula kupita kiasi angalau mara moja kwa wiki kwa miezi 3

  • Kujisafisha tumbo ili kurekebisha kula kupita kiasi kwa kufanya vitu kama vile kujitapisha

Je, madaktari hutibu bulimia vipi?

Madaktari hutibu bulimia kwa ushauri nasaha na dawa.

Ushauri nasaha unaweza kuwa wa mmoja-mmoja na tabibu au katika kikundi. Malengo ni:

  • Kukuchochea ubadilike

  • Kuanzisha utaratibu wa kula wa kawaida na unaoweza kubadilika

  • Kupunguza umakini wako wa uzani na umbo la mwili

Madaktari wanaweza kukuandikia aina ya dawa ya kupunguza unyogovu ili kusaidia kupunguza mara ngapi unazokula na kusafisha tumbo. Dawa hii pia hutibu wasiwasi na unyogovu, hali ambazo ni kawaida kwa watu wenye bulimia.