Mkakamao wa Misuli

Imepitiwa/Imerekebishwa Sept 2023

Mkakamao wa misuli ni nini?

Mkakamao wa misuli ni maumivu kwenye misuli yako inapokaza kwa ghafla. Mkakamao wa misuli hudumu kwa sekunde chache au dakika kadhaa.

  • Mkakamao wa misuli hufanyika bila kutarajiwa

  • Mikakamao ya misuli hutokea kwa kawaida kwa watu wenye afya nzuri, hususan watu wenye umri wa makamo na watu wazee

  • Mikakamao inaweza kufanyika wakati au punde baada ya mazoezi mazito au ukiwa kitandani usiku

  • Kwa nadra, mikakamao ya misuli huwa dalili ya tatizo la neva

Ni nini husababisha mkakamao wa misuli?

Sababu za kawaida za mikakamao ya mishuli:

  • Mikakamao isiyo hatari inayotokea bila sababu

  • Mazoezi (ama wakati wa mazoezi au punde baadaye)

Una uwezekano mkubwa zaidi wa kupata mikakamao iwapo:

  • Misuli yako ya sehemu ya chini ya nyuma ya mguu imekaza kwa kutojinyoosha

  • Unaketi kwa vipindi virefu

  • Huna madini ya kutosha (elektroliti) hali inayoweza kutokea iwapo unatumia diuretiki (vidonge vya maji), uko katika miezi ya mwisho ya ujauzito wako, au una matatizo kama vile upungufu wa vitamini D au tatizo la unywaji wa pombe

  • Unapatiwa huduma ya kusafisha damu kutokana na matatizo ya figo

  • Tezi dudumio haitengenezi homoni ya kutosha (dundumio lisiloamilifu)

  • Unatumia dawa fulani

Je, ninapaswa kumwona daktari lini kuhusiana na mikakamao ya misuli?

Nenda kwa daktari mara moja ikiwa una mkakamao wa misuli na mojawapo ya ishara hizi za tahadhari:

  • Maumivu kwenye kifua, mikono au tumbo yako

  • Udhaifu au kupoteza uwezo wa kuhisi kwenye sehemu za mwili wako

  • Mitetemo ya misuli

  • Mikakamao ilianza baada ya kupoteza majimaji mengi ya mwili kutokana na kutapika, kutokwa na jasho sana, kuendesha, au kutumia diuretiki (dawa zinazokufanya ukojoe zaidi)

Mpigie daktari wako simu ndani ya siku 1 hadi 2 iwapo:

  • Unapata mikakamao ya misuli ya miguu unapotembea ambayo inaisha mara tu ukiacha kutembea

  • Mikakamao yako ilianza baada ya kuanza kutumia dawa mpya

  • Unakunywa pombe kwa kiasi kikubwa

Je, nitarajie nini ninapokwenda kumwona daktari wangu?

Daktari wako atakuuliza kuhusu dalili zako na kukufanyia uchunguzi wa kimwili.

Wakati mwingine, madaktari watafanya vipimo vya damu ili kuangalia iwapo una matatizo mengine ambayo huenda yanasababisha dalili zako.

Madaktari hutibu vipi mikakamao ya misuli?

Ikiwa tatizo lingine la kiafya linasababisha mikakamao yako, madaktari watatibu tatizo hilo.

Ikiwa mikakamao yako haina madhara lakini inasababisha maumivu, unaweza kupunguza maumivu kwa:

  • Kunyoosha musuli

Kwa mfano, ikiwa mkakamao umetokea kwenye sehemu ya chini ya nyuma ya mguu, nyoosha sehemu hiyo kwa kuvuta vidole vyako vya mguu kuelekea juu (mbinu ya kujinyoosha ya mkimbiaji au gastrocnemius).

Ninawezaje kuzuia mikakamao ya misuli?

  • Nyoosha misuli yako kabla ya kufanya mazoezi au kwenda kulala

  • Baada ya kufanya mazoezi, kunywa maji na viowevu vingine (hususan vinywaji vya spoti, vilivyo na elektroliti)

  • Usifanye mazoezi mengi mazito baada ya kula