Ugonjwa wa Hisia Mseto

(Tatizo la Unyogovu Kupita Kiasi)

Imepitiwa/Imerekebishwa Oct 2023

Ugonjwa wa hisia mseto ni nini?

Ugonjwa wa hisia mseto ni tatizo la akili ambalo lina vipindi vya mfadhaiko na vipindi vya uchangamfu.

Mfadhaiko ni kuhisi huzuni nyingi hivi kwamba huwezi kufanya shughuli za kila siku au hivi kamba hutaki kufanya vitu ambavyo ulifurahia kuvifanya hapo awali.

Uchangamfu ni hali ambapo una hamasa na kujiamini kwa kiwango kikubwa, mawazo yako yanavurugwa kwa urahisi, na unafanya maamuzi hatarishi.

  • Ugonjwa wa hisia mseto kwa kawaida huanza ukiwa kijana au katika miaka ya 20 au 30

  • Kuna uwezekano kuwa ugonjwa wa hisia mseto ni wa kurithishwa katika familia

  • Hali yako mara nyingi itakuwa ya kawaida wakati hauna kipindi cha mfadhaiko au uchangamfu

  • Madaktari hutibu ugonjwa wa hisia mseto kwa kutumia dawa na matibabu ya kisaikolojia

Kuna aina 2 za ugonjwa wa hisia mseto, hisia mseto 1 na hisia mseto 2.

Ikiwa una ugonjwa wa hisia mseto 1, unapata:

  • Angalau kipindi 1 cha uchangamfu kinachokuzuia kufanya shughuli za kila siku na kinaweza kujumuisha maono ya uwongo (wakati ambapo unashindwa kujua vitu vya kweli)

  • Kwa kawaida vipindi vya mfadhaiko

Ikiwa una ugonjwa wa hisia mseto 2, unapata:

  • Angalau kipindi 1 cha uchangamfu usiokithiri (uchangamfu mdogo)

  • Vipindi vya mfadhaiko mbaya

Je, ni nini husababisha ugonjwa wa hisia mseto?

Madaktari hawajui haswa kinachosababisha ugonjwa wa hisia mseto. Jeni zako (maelezo ya kijenetiki unayopata kutoka kwa wazazi na mababu zako) zinaweza kuchangia.

Nyakati za uchangamfu (vipindi vya kuchangamka) zinaweza kuchochewa na

  • Kuongezeka au kupungua kwa kemikali fulani (visafirishaji ujumbe au ishara vya neva) katika mwili wa mtu—visafirishaji ujumbe au ishara vya neva ni kemikali kama vile serotonin na norepinephrine ambazo seli za neva hutumia kutuma ujumbe kwenye ubongo na mwili

  • Uvimbe wa ubongo au matatizo mengine ya ubongo

  • Tukio la mfadhaiko

  • Dawa za kulevya, kama vile kokeni

  • Matatizo mengine ya kiafya, kama vile matatizo ya tezi dudumio

Ni zipi dalili za ugonjwa wa hisia mseto?

Nyakati (vipindi) za mfadhaiko au uchangamfu huja na kutoweka. Hapo katikati, hali yako inaweza kuwa ya kawaida. Vipindi vya mfadhaiko na uchangamfu vinaweza kudumu kwa wiki kadhaa au hadi miezi 6.

Dalili za mfadhaiko:

  • Kuhisi huzuni sana

  • Kupungua kwa hamu ya kushiriki katika shughuli, hata zile ulizokuwa ukizipenda zamani

  • Kufikiria na kutembea polepole

  • Kuhisi majisuto na kukosa matumaini

  • Kulala kwa muda mrefu kuliko kawaida

  • Kuona vitu ambavyo si vya kweli

Dalili za uchangamfu:

  • Hisia ya kujiamini sana na kufikiria kuwa unaishi maisha mazuri

  • Kuwa na hamasa kubwa

  • Kuudhika haraka

  • Kulala kwa muda mfupi kuliko kawaida

  • Kuongea zaidi

  • Kuvurugwa mawazo kwa urahisi na kubadilisha kutoka kwa shughuli moja hadi nyingine

  • Kushiriki katika shughuli hatarishi, kama vile kamari au ngono, bila kufikiria kuhusu athari zake

  • Wakati mwingine kuona na kusikia vitu ambavyo si vya kweli

Watu walio na vipindi vya uchangamfu uliokithiri (ukichaa kupita kiasi) wanaweza kuwa na dalili kama vile:

  • Imani potofu kuwa wao ni watu wa kipekee, kama vile kuwa wao ni yesu au wana kipaji maalum

  • Kufikiria kuwa watu wanawafuata

  • Shughuli kupita kiasi, kama vile kukimbia huku na kule, kupiga mayowe, na kuimba

  • Kutotenda au kutofikiria kwa busara

Watu walio na uchangamfu kupita kiasi wanahitaji kwenda hospitalini mara moja.

Madaktari wanawezaje kujua iwapo nina ugonjwa wa hisia mseto?

Madaktari wanashuku kuwa una ugonjwa wa hisia mseto kulingana na mtindo wa dalili zako. Ukiwa na tatizo la uchangamfu kupita kiasi, huenda usiweze kuripoti dalili zako kwa usahihi kwa sababu hufikiri kuwa una tatizo lolote. Kwa hivyo madaktari wanaweza kuomba maelezo kutoka kwa wanafamilia.

Madaktari wanaweza pia kufanya vipimo vya damu au mkojo ili kuangalia iwapo dawa au matatizo mengine ya kiafya yanasababisha dalili zako.

Madaktari hutibu vipi ugonjwa wa hisia mseto?

Huenda daktari:

  • Kupendekeza dawa, kama vile lithium au valproate

  • Kutoa usaidizi wa ushauri nasaha wa kibinafsi au vikundi (matibabu ya kisaikolojia)

  • Dawa zisiposaidia tatizo lako la mfadhaiko, watakupatia tiba ya mshtuko wa umeme (ambayo awali iliitwa tiba ya kushtua ubongo)

Katika tiba ya mshtuko wa umeme, daktari wako atakupa dawa ili ulale kisha atapitisha umeme kwenye ubongo wako. Madaktari hawajui kwa nini, lakini umeme mara nyingi husaidia kuondoka mfadhaiko.

Ikiwa una tatizo la uchangamfu au mfadhaiko kupita kiasi na unafanya vitendo hatarishi vinavyoweza kusababisha matatizo mabaya, madaktari wanaweza kukutibu hospitalini